Habari
Serikali yataka ulinzi na uhifadhi wa Ziwa Victoria
Serikali imesisitiza umuhimu wa ulinzi wa ziwa Victoria kwa maendeleo ya wananchi.
Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb) amesema hayo katika maadhimisho ya kwanza ya Siku ya Ziwa Victoria yaliyofanyika katika viwanja vya Nanenane Nyamhongolo jijini Mwanza,.
Dkt. Mwigulu, mgeni rasmi wa siku hiyo, amesema ziwa Victoria ni rasilimali ya pamoja inayopaswa kulindwa na kuhifadhiwa kwa ushirikiano wa kikanda kutokana na mchango wake mkubwa katika uchumi, biashara, mazingira, usalama na maisha ya wananchi.
“Ziwa Victoria si mali ya nchi moja. Ni rasilimali inayotuunganisha kama jumuiya na tunapaswa kushirikiana katika kulinda mazingira, usalama na uchumi unaotegemea ziwa hili,” Dkt. Nchemba amesema.
Amesema maadhimisho hayo yanapaswa kuwa sehemu ya kuhamasisha usimamizi endelevu wa rasilimali za maji, kuimarisha mshikamano wa kikanda pamoja na kuongeza uwajibikaji wa pamoja katika kulinda mazingira ya ziwa Victoria kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Amesisitiza umuhimu wa kuimarishwa kwa mifumo ya usalama na uokoaji majini pamoja na matumizi ya teknolojia za kidijitali katika kufuatilia shughuli za uvuvi, ubora wa maji na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Ametoa wito kwa taasisi za utafiti kuendelea kufanya tafiti zitakazosaidia kupata suluhisho la changamoto zinazoathiri mazingira ya ziwa Victoria ikiwemo ongezeko la magugu maji na uharibifu wa vyanzo vya maji.
Aidha, Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) amesema Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maji katika Kanda ya ziwa pamoja na kuimarisha juhudi za kulinda na kuhifadhi ziwa Victoria ambalo ni nguzo muhimu ya uchumi, usalama na maendeleo ya wananchi.
Sanjari na hayo Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Mwajuma Waziri amesema Tanzania imekuwa mwenyeji wa kwanza wa maadhimisho hayo kufuatia maamuzi ya Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Amesema maadhimisho hayo yamehusisha shughuli mbalimbali ikiwemo kuotesha miti, maonesho ya wadau wa Sekta ya Maji pamoja na mijadala kuhusu uhifadhi wa Ziwa Victoria.

