Habari
Prof. Jamal akitaka Chuo cha Maji kuongeza somo la ujasiriamali
Katibu Mkuu, Wizara ya Maji Prof. Jamal Katundu ameutaka uongozi wa Chuo cha Maji na Bodi ya Chuo hicho kukiimarisha Chuo katika utafiti,ushauri na mafunzo ya ujasiriamali ili kukiimarisha Chuo,Wakufunzi na kuendelea kuzalisha wahitimu walio bora zaidi.
Katibu Mkuu Prof. Katundu amemuwakilisha Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) katika Mahafali ya 47 ya Chuo cha Maji yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimaji City Jijini Dar es Salaam.
Akizungumzia miradi ya uendelezaji wa miundombinu ya Chuo cha Maji cha Jijini Dar es Salaam, Prof. Katundu amesema ukarabati na ujenzi wa miundombinu takribani 32 ya majengo ya Utawala,Maktaba,Mabweni na Madarasa yanayogharimu shilingi bilioni 7.5 kutoka serikali kuu yatakamilika kwa wakati.
Aidha Prof. Katundu amemuagiza Mkuu wa Chuo cha Maji,Dkt. Adam Karia kuweka utaratibu wa mafunzo kwa vitendo kwa Vijana 682 waliohitimu kwa kuwapeleka katika Mamalaka za Maji nchini kupata ujuzi katika fani zao baada ya masomo ya darasani.
Pamoja na hayo amekitaka chuo kusimamia kwa nguvu jukumu la kuwaandaa vijana katika fani mbalimbali za Sekta ya Maji.
Kitengo cha Mawasiliano