Habari

Imewekwa: Mar, 11 2023

Mradi wa maji wa Miji 28 kuimarisha huduma ya maji Songea

News Images

Wizara ya Maji imesaini mkataba na Mkandarasi kampuni ya China Civil Engineeering Construction Corporation (CCECC) ili kujenga mradi wa maji wa Miji 28 katika Mji wa Songea wenye thamani ya Tshs bilioni 145.7.

Naibu Waziri wa Maji Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb) akimwakilisha Waziri wa Maji amesema mradi huo ukikamilika utakua na uwezo wa kuzalisha maji kutoka lita milioni 11.58 kwa siku hadi kufikia lita milioni 42.581 kwa siku.

Amesema mradi huo utamaliza kero ya maji katika Manispaa ya Songea kwa sababu upatikanaji wa maji utakua wa uhakika na utakuwa na uwezo wa kuwahudumia wananchi zaidi ya laki nne.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji Mhandisi Nadhifa Kemikimba akizungumza kabla ya kusaini mkataba huo amesema mradi huo utakapokamilika utakuwa na uwezo kuhudumia wananchi wa Songea hadi mwaka 2045, ambapo idadi ya wakazi wa Songea inatarajiwa kuwa zaidi ya 400,000.

Amezitaja kazi ambazo zitafanyika kwenye mradi huo kuwa ni ujenzi wa bwawa lenye uwezo wa kujaza maji lita milioni 4.8, ujenzi wa mtambo wa kuchuja maji lita milioni 16 kwa siku, ujenzi wa matanki 10 yatakayosafirisha maji kutoka kwenye bwawa hadi kwenye matenki pia usambazaji wa maji wenye kilometa zaidi ya laki nne.

Hafla hiyo ilihushuhudiwa na maelfu ya wananchi pamoja na viongozi mbalimbali wa mkoa.

Kitengo cha Mawasiliano