Habari
Waziri Mkuu awataka Wizara ya Maji kutumia mitambo ya kuchimba visima kuharakisha utekelezaji wa miradi
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba amesisitiza matumizi ya mitambo ya kuchimba visima iliyonunuliwa na serikali kutumika kwa ajili ya kutatua changamoto ya huduma ya maji kwa watanzania.
Agizo hilo amelitoa akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Rukwa. Amesema serikali imenunua mitambo hiyo 25, mitambo ya kuchimba mabwawa pamoja na ile kupima maji baada ya kuona mahitaji ya haraka katika utekelezaji wa miradi ya maji.
Amesitiza kuwa mitambo hiyo haitakuwa na maana iwapo serikali bado itaendelea kukodi mitambo wakati inayo mitambo yake hivyo wizara ihakikishe inaweka mipango imara ya kutumia mitambo hiyo katika utekelezaji wa miradi.
Amekumbusha agizo lake la kuhakikisha vituo vyote vya huduma za jamii vinafikishiwa huduma ya majisafi na salama ndani ya miezi sita na kusisitiza kuwa atachukua hatua kwa yeyote atakayepuuza agizo hilo.
Mitambo hiyo ilinunuliwa na serikali ya awamu ya sita katika muhula wa kwanza wa utawala na kuitawanya mikoa yote ya Tanzania ili kuharakisha adhma ya serikali ya kutatua changamoto ya huduma ya majisafi na salama kwa watanzania.

