Habari

Imewekwa: Mar, 13 2026

​SERIKALI YATUMIA BILIONI 16.5 KUNUNUA PAMPU ZA RUVU JUU NA CHINI, HUDUMA YA MAJI KUIMARIKA ZAIDI

News Images

Serikali imetumia Shilingi Bilioni 16.5 kununua pampu mpya za kusukuma maji kwa ajili ya mitambo ya Ruvu Juu na Ruvu Chini, inayohudumia wakazi wa Jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani.

Hatua hiyo inalenga kuimarisha huduma ya usambazaji wa maji kwa wananchi na kuongeza uhakika wa upatikanaji wa maji safi na salama kwa wateja wa maeneo hayo.

Zoezi la ufungaji wa pampu hizo linatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2026.

Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso (Mb), akiongozana na wataalam wa Sekta ya Maji, akiwa katika ziara ya kikazi nchini China, wameshuhudia majaribio ya mwisho ya awamu ya pili ya pampu hizo katika kiwanda cha KSB kilichopo jijini Shanghai.

Baada ya kushuhudia majaribio hayo, Waziri Aweso ameridhishwa na ubora pamoja na viwango vya pampu hizo na kuidhinisha kuanza kwa taratibu za usafirishaji wake kuja nchini mara baada ya kukamilika kwa maandalizi yote muhimu.

Aidha, awamu ya kwanza ya pampu hizo yenye jumla ya pampu nne tayari imekamilika na imewasili nchini, ambapo kazi ya ufungaji imeanza katika mitambo husika.

Kazi ya Ununuzi wa pampu hizo ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuimarisha huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani kupitia maboresho ya miundombinu ya maji.

Kitengo cha Mawasiliano