Habari
Waziri wa Maji Atoa Miezi Mitatu kwa Mamlaka za Maji Kufunga Dira za Maji kwa Wateja

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Waziri wa Maji, Mhe. Profesa Makame Mbarawa (Mb) amezipa mamlaka za maji zinazotumia bei za kukadiria (flat rates) miezi mitatu kuhakikisha wateja wote wamefungiwa dira za maji ili kila mteja alipe gharama ya maji kwa kiasi alichotumia. Pia ameziagiza mamlaka za maji za mikoa kuhakikisha wanadhibiti upotevu wa maji na kuongeza mtandao wa maji ili kujiongezea mapato.
Profesa Mbarawa alitoa maagizo hayo alipokuwa anafanya uzinduzi wa mradi wa maji wa Kijiji cha Shilima kata ya Kikumbiji, Wilayani Kwimba Mkoa wa Mwanza.
Hii ni awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi wa maji katika Vijiji vya Shilimia, Mhande na Izizimba. Mradi wa maji wa Shilima ulianza kutekelezwa mwaka 2013 na ulitakiwa kukamilika katika kipindi cha miezi sita. Hata hivyo, kutokana na udhaifu wa Mkandarasi pamoja na usimamizi mbaya haukuweza kukamilika.
Waziri Mbarawa tarehe 3 Julai, 2019 akiwa katika ziara ya kikazi Wilayani Kwimba alitoa ahadi ya kukamilisha mradi huo kwa kutumia wataalamu wa ndani kwa kuhakikisha wananchi wa Kijiji cha Shilima wanapata maji katika kipindi cha miezi miwili, yaani hadi kufikia tarehe 3 Septemba, 2019, ahadi ambayo ilikamilika tarehe 25 Agosti, 2019 siku tisa kabla ya tarehe ya makubaliano.
Alipokuwa akisoma taarifa ya Mradi, Meneja wa RUWASA Wilaya ya Kwimba Mhandisi Boaz Matundalo alisema kuwa, Kijiji cha Shilima kina wakazi wapatao 7,526 ambapo mradi huu wenye magati 35 una uwezo wa kuhudumia wakazi 8,750 ikiwa ni wastani wa watu 250 kwa kila gati.
Maradi wa maji wa Shilima umetekelezwa na wataalamu wa ndani kutoka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA).
Kitengo cha Mawasiliano
14 Septemba, 2019