Habari

Imewekwa: Feb, 10 2026

Mifumo ya Ununuzi Izingatiwe Kuharakisha Utekelezaji wa Miradi ya Maji

News Images

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Mwajuma Waziri, amesisitiza umuhimu wa kuzingatia na kutumia ipasavyo mifumo ya ununuzi wa umma, hususan mfumo wa NeST, ili kupunguza malalamiko kutoka kwa wadau wa Sekta ya Maji wakiwemo wakandarasi na hivyo kuharakisha utekelezaji na ukamilishaji wa miradi ya maji kwa wakati.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Sheria wa Wizara ya Maji, Wakili Msomi Simon Nkanyemka, kwa niaba ya Katibu Mkuu, wakati akifungua mafunzo ya siku tano yaliyolenga Menejimenti na wataalamu wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA). Amesema mafunzo hayo ni muhimu kwani matumizi sahihi ya mfumo wa NeST yanarahisisha utekelezaji wa shughuli za umma, kuongeza uwazi na uwajibikaji, pamoja na kuimarisha imani ya Serikali kwa wadau wake na wananchi wanaonufaika na huduma za maji.

Aidha, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa RUWASA, Titus Mkapa, akimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, ametoa wito kwa viongozi na watumishi wa RUWASA kuhakikisha wanatumia mfumo wa NeST mara kwa mara kama sehemu ya utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Amesisitiza kuwa nidhamu ya matumizi ya mfumo huo ni msingi wa kuondoa ucheleweshaji wa taratibu za ununuzi na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa miradi.

Awali, Mkurugenzi wa Ununuzi wa RUWASA, Joseph Macha, amesema mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo wajumbe wa Menejimenti pamoja na wataalamu mbalimbali wakiwemo Maafisa Ununuzi kuhusu matumizi ya mfumo wa NeST, pamoja na utekelezaji wa Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2023 na kanuni zake. Ameongeza kuwa uelewa sahihi wa sheria na mifumo ya ununuzi ni nguzo muhimu katika kuhakikisha miradi ya maji inatekelezwa kwa viwango