Habari
Bil. 24.4 kufanikisha huduma ya majisafi Tinde - Shelui

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Philip Isdor Mpango ameweka jiwe la msingi la mradi wa maji wa Ziwa Victoria kwa mji wa Tinde. Hafla ya hiyo imefanyika leo Januari 19, 2023 katika eneo la tanki la maji la Buchama nje kidogo ya mji wa Tinde mkoani Shinyanga.
Mradi utagharimu shilingi bilioni 24.4, na unatarajia kuhudumia wakazi wa miji ya Tinde na Shelui.
Mhe. Dkt.Mpango amesema dhamira ya serikali ya awamu ya sita ni kuhakikisha inatekeleza miradi ambayo itawezesha huduma endelevu ya majisafi na hivyo kusaidia kukuza uchumi wa Taifa.
Amewataka wadau wa sekta ya maji kuongeza weledi katika usimamizi wa miradi ya maji pamoja na utunzaji wa rasilimali za maji ili kuwezesha lengo la serikali la kuifanya miradi hiyo iwe endelevu.
Kwa upande wake Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) amesema Wizara itaendelea kufuatilia na kusimamia kwa makini utekelezaji wa miradi ya maji ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati na kutoa huduma kwa wananchi.
Kitengo cha Mawasiliano