Habari
Wakandarasi wa Mradi wa Maji wa Tabora - Igunga- Nzega Watakiwa Kuongeza Kasi

Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maji Mhandisi Anthony Sanga amewataka wakandarasi wanaojenga mradi wa maji wa Tabora – Igunga – Nzega kuongeza kasi ya ujenzi ili kukamilisha mradi kwa wakati.
Mhandisi Sanga ametoa maelekezo hayo alipotembela na kuona hatua iliyofikiwa ya ujenzi katika mradi huo hivi karibuni.
Naibu Katibu Mkuu Mhandisi Sanga alisema pamoja na maendeleo ya mradi kuridhisha, aliwataka wakandarasi kuhakikisha wanajenga miundombinu itakayofikisha huduma ya maji kwa wananchi badala ya kuweka nguvu zaidi katika majengo.
“Wananchi wamesubiri mradi huu kwa muda mrefu, kazi zilizobaki hakikisheni zinaisha haraka hasa za kupeleka huduma kwa wananchi, kazi kama kupaka rangi majengo zisubiri hadi wananchi wapate huduma ya maji” Mhandisi Sanga alisema.
Kwa upande wao, wakandarasi walipokea maelekezo hayo na kuahidi kukamilisha kazi zote muhimu kwa wakati kwa kufanya kazi kwa saa 24.
Mradi wa maji wa Tabora – Igunga – Nzega ambao una gharimu kiasi cha shilingi bilioni 602, unajengwa na kampuni tatu kutoka nchini India ambazo ni Megha Engineering Infrastructures, L & T na Afcons. Mradi ukikamilika utanufaisha idadi ya wananchi milioni moja na laki mbili. Chanzo cha mradi ni Ziwa Viktoria.
Kitengo cha Mawasiliano